Wednesday, December 18, 2013

Tukumbushane Wadau




Kwanza nawapongeza wapiganaji wote tunaoendelea kufanya kazi ya uandishi wa habari ambayo kimsingi ni kazi ya kiutumishi kwa umma.

Naomba tuendelee kutumikia umma wa watanzania na tuendelee kuandika habari zenye maslai kwa umma. Kwangu mimi utumishi wetu utakua na maana na manufaa kwa watanzania kama tutaandika, kutangaza, kuonesha na kuchapisha habari, taarifa na matangazo yenye kuitetea Tanzania na watu wake.

Kwenye kazi ya kuitetea Tanzania na watu wake tusisahau kwamba zipo taarifa nyingine ama habari nyingine licha ya ukweli wake na ubora wake zina madhara kwa Tanzania na watu wake, kwa aidha kuichafua nchi usoni kwa mataifa mengine ama zinawaathiri watanzania.

Naamini tunayajua haya na wengi tunayatekeleza, hebu tuendelee kufanya hivyo na wale wasiofanya oneni umuhimu wa kufanya hivyo ili Tanzania iwe mahali salama pa kuishi na watanzania wafurahie maisha yao licha ya kuwepo kwa changamoto nyingi ikiwemo umasikini.

Tukiwa tunakumbushana hili hebu pia tukumbushane umuhimu wa kuzingatia weledi, maadili, haiba na staha ya mwandishi wa habari. Tusione haya kujifunza, tusione makosa kukosoana na isiwe hatari kukubali pale unaposhindwa.

Nasema hivyo kwa sababu wapo baadhi yetu ambao kimsingi hata wao wanajua kwamba kazi hii haiendani nao lakini wanalazimisha, matharani kuwa watangazaji bila kujali ubora wa sauti, rafudhi na uwezo wao kiutangaza, wapo wanaofanya uchambuzi magazetini kwenye redio na Televisheni bila kujali kama uchambuzi wao hauna utafiti wa kutosha wala mpangilio, wapo wanaokwenda kukusanya habari bila kujali muonekana wao mbele ya jamii na tabia zao kama zinafanana na kioo cha jamii na wapo wanaochapisha magazeti na vijarida bila kujali yale wanayochapisha kama yana tija ama la.

Nasema bahati nzuri, haya ninayosema sie wenyewe wahusika tunayajua, nashauri tupime wenyewe na kuchukua hatua kabla ya kuhukumiwa na jamii ama kusubiri tupigiwe kelele.

Na sasa tunakwenda kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa na baadaye Uchaguzi Mkuu na tayari hekaheka zimeanza leo, nashauri tutumie kalamu zetu kukataza hekaheka hizi kwa sababu zina madhara kwa taifa, muda wake bado japo wapo watakaonikosoa. Tunaliacha taifa liwe linatumia muda mrefu kujadili uchaguzi badala ya maendeleo, tunaliacha taifa ligubikwe na ajenda ya siasa badala ya kupambana na umasikini unaowatafuna watanzania wengi, tunaacha watu wachache wanaotetea maslai yao kuliyumbisha taifa na mwishowe tunawaacha watanzania washindwe kutengeneza ajenda za nchi yao. Ndio, ni sisi waandishi wa habari tunaopaswa kuwajibika kwa hili anayekataa atupishe.

Napiga la Mgambo nikiomba waandishi wenzangu tuwe chanzo cha matumaini kwa watanzania, tusiache nchi ikitupiwa mawe ndani na nje, tusiache matatizo ya watanzania yakawa donda ndugu, na tuwaongoze watanzania kukataa jambo lolote linaloigharimu nchi na watu wake kwa njia ya amani.

Mwisho nawapenda sana na Aluta Continua………..