Friday, March 29, 2013

KESHO KIBARUA KIKALI CHA NDUGU WAWILI DIMBA LA KAITABA!

SONY DSC
By Baraka Mpenja
Ni vita ya kufa na kupona kati ya watengeneza sukari nchini Tanzania klabu ya Mtibwa Sugar dhidi ya Kagera Sugar watakaokuwa na kazi ngumu ya kuwania pointi tatu muhimu katika mchezo wa ligi kuu  soka Tanzania bara.
Pambano hilo la watengeneza sukari sukari limevuta hisia za mashabiki lukuki wa soka kwa mikoa ya kanda ya ziwa Victoria  huku likitarajiwa sehemu ya kufurahia katika mapumziko ya pasaka.


Akizungumza kutoka mkoani Kagera, kocha mkuu wa Mtibwa sugar na nahodha wa zamani wa timu hiyo pamoja na timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars), mzalendo Merck Mexeme amesema maandalizi ya mchezo huyo yamefanyika kwao Manungu na leo hii wanapasha moto misuli baada ya safari ndefu ya siku mbili kuelekea mkoani humo.
Mexme alisema soka siku zote ni maandalizi, wao wamejipanga vizuri na bahati nzuri hakuna mchezaji ambaye yuko hatarini kuukosa mchezo huo unaotabiriwa kuwa mgumu sana.

“Kagera ni timu nzuri na wana kocha mzuri, mzee Abdallah King Kibadeni ambaye alinifundisha hata mimi, ana mbinu nyingi sana lakini kwa kuwa aliwahi kuwa mwalimu wangu, nitatumia mbinu zake kumfunga akiwa nyumbani kwake hapo kesho”. Alisema kocha Mexeme .
Mexeme ambaye ni kocha aliyejijengea heshima kubwa akiwa mchezaji na sasa kocha wa Mtibwa sugar aliongeza kuwa kesho atapanga kikosi chake cha matumaini na anawapanga vijana wake kupambana na Kagera Sugar ambao watakuwa mbele ya umati mkubwa wa mashabiki ambao ndio siri ya matokeo unapocheza uwanja wa nyumbani.

Naye mshambuliaji mahiri wa tanzania miaka ya nyuma huku akivuma na kupewa jina la king Mputa akiwa na klabu ya Simba akicheza kama winga mahiri miaka ya sabini na sasa ni kocha wa watengeneza miwa pacha wa mtibwa, Kagera Sugar “ wanangulukumbi”  Abdallah Kibaden akiongea kwa kujiamini baada ya kutoa dozi kwa simba SC amesema kuwa mchezo wao wa kesho wanataraji kuwapa zawadi ya pasaka mashabiki wao.

 “Mara baada ya kuifunga simba goli 1-0, vijana wangu wana kila sababu ya kuongeza wigo wa tofauti ya pointi kati yetu na Mtibwa  ,Wanahitaji sana ushindi katika mchezo wa kesho, malengo yetu ni kupata nafasi mojawapo ya kuwakilisha nchi  medani ya kimataifa”. Alisema king Mputa.
Nao mabingwa watetezi wa taji wekundu wa Msimbazi Simba “Taifa Kubwa” baada ya kipigo cha 1-0 sasa watakuwa na kazi pevu katika nyasi nzuri za uwanja wa CCM Kirumba kudadavuana na watoto wa mitaa ya Kishamapanda Toto Africa.

 Simba  watashuka Kirumba wakitaka kuonesha uwezo wao na manjonjo ya vijana wake mbele ya mapacha hao wa vinara wa ligi kuu ya kandanda Tanzania bara, klabu ya Yanga ya Dar es Salaam.
Tayari timu tatu za Mbeya city ya jijini Mbeya, Ashant United ya Dar es Salaam  na Rhino Rangers ya Tabora zimeshakata tiketi ya kucheza mitanange ya ligi  kuu msimu ujao, huku timu tatu za ligi zikisubiri kupitiwa na fagio la chuma.
Timu za African Lyon, Polisi Morogoro, JKT Ruvu, Tanzania Prisons, Mgambo shooting na JKT Oljoro zinaonekana kuchuana vikali kukwepa mkasi wa kurejea ligi daraja la kwanza Tanzania bara (FDL).