Saturday, July 6, 2013

Tunduru watakiwa kutunza na kuhifadhi mazingira

Mkuu wa wilaya ya Tunduru Chande Nalicho
------------------------------------------ 
Na Nathan Mtega,Tunduru

Serikali wilayani Tunduru mkoani  Ruvuma imewataka wananchi na viongozi wa serikali na vyama vya siasa wilayani humo kutambua kuwa jukumu la uhifadhi na utunzaji  wa mazingira ni la kila mmoja kwa sababu madhara ya uharibifu wa mazingira yanaathiri kila kundi.


Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa wilaya ya Tunduru Chande Nalicho wakati akifungua  mdahalo  wa wazi wa mchakato wa kukusanya maoni ya wananchi  juu ya uhifadhi wa mazingira na mabadiliko ya hali ya hewa ambapo amesema tabia , shughuli za kibinadamu na mabadiliko ya hali ya hewa ni vitu vinavyochangia uharibifu wa mazingira kwa kiasi kikubwa.


Amesema kuwa mdahalo  huo unaoendeshwa na asasi ya kiraia ya mazingira Tunduru kwa ufadhili wa asasi ya The foundation  for  civil  society  una lengo kubwa la kuikoa wilaya Tunduru dhidi ya uharibifu wa mazingira unaozidi kuongezeka siku hadi siku.


Amesema kuwa shughuli mbali mbali za kibinadamu pamoja na kilimo kisichozingatia ushauri wa kitaalamu ambacho huhusisha kilimo cha kuhama hama kinachofanywa na baadhi ya wananchi wa wilaya hiyo huku wataalamu wa sekta ya kilimo wakishuhudia bila kuchukua hatua za kutoa elimu na ushauri wa matumizi bora ya ardhi ni sababu zinazosababisha kuendelea kuwepo kwa uharibifu wa mazingira siku hadi siku.


Akiongoza mdahalo huo mwezeshaji Thomas Lima amesema kuwa sera ya taifa ya mazingira  inasisitiza umuhimu wa utunzaji wa mazingira lakini elimu zaidi kwa wananchi na sheria za utunzaji na uhifadhi wa mazingira vinapaswa kuzingatiwa kwa sababu sekta ya uhifadhi wa mazingira imekuwa ikifadhiliwa kwa gharama kubwa na wafadhili wa ndani na nje ya nchi.


 Amesema kuwa suala la uhifadhi wa mazingira linapaswa kupewa kipaumbele kuanzia ngazi ya familia ili kuwajengea watoto utamaduni wa kuyapenda na kuyatunza mazingira yanayowazunguka kwa sababu moja ya sababu zianazochangia kuendelea kuwepo kwa uharibifu mkubwa wa mazingira ni pamoja na ukosefu wa elimu ya uhifadhi na utunzaji wa mazingira kwa wananchi walio wengi na hasa waliopo maeneo ya vijijini ambako hutumia kuni kama nishati kwa kukata miti bila kupanda.


Akizungumza mratibu wa asasi hiyo ya kiraia ya mazingira Tunduru John Nginga amesema kuwa mdahalo  huo  uliofunguliwa  na mkuu wa wilaya hiyo ya Tunduru  utafanyika katika majimbo mawili yaliyopo wilayani Tunduru ambayo ni Tunduru kaskazini na Tunduru kusini kwa lengo la kuikoa wilaya hiyo na uharibifu wa mazingira unaozidi kukua kwa kasi kubwa siku hadi siku.


Habari kwa hisani ya demashonews