Thursday, May 23, 2013

Balaa hili la Vituo vya Kuchimba dawa, Dr Harrison Mwakyembe unalijua?

Licha ya kwamba kituo cha kuchimba dawa cha Lugono kilichopo kilometa chache kutoka Morogoro Mjini kwenda mikoa ya kusini, kimepata mwekezaji wa kujenga choo cha kulipia lakini choo hicho hakina uwezo wa kutosha kuhudumia japo basi moja la abiria na hivyo abiria hulazimika kuchimba dawa porini, nje ya jengo la mwekezaji huyo ili wasichelewe na kuachwa na basi. kwa lugha nyingine ni kama vile mwekezaji huyo kapewa dili tu ya kupata pesa lakini huduma ni mbaya kupita maelezo. Dr Harison Mwakyembe unalijua hili?
Hapa Abiria wanasongamana kwenye sehemu moja finyu kwa ajili ya haja ndogo katika kituo cha kuchimba dawa cha Lugono Morogoro. Dr Mwakyembe upo?

Abiria wengine wakisubiri nje kutokana na jengo la kujisaidia kuhemewa licha ya kwamba wanaokwenda kuchimba dawa hilipia fedha

Hapo Jamaa anakusanya shilingi 200 kwa kila abiria anayetaka kujisadia (kuchimba dawa) bila 200 huchimbi dawa labda ukimbilie porini mbali na lilipo jengo hilo

Abiria wakitoka Porini walikokwenda kuchimba dawa licha ya kulipia shilingi 200 kwa kila mmoja.

Tena kituo hiki kina baraka zote za serikali ya wilaya ya Mvomero

Kando ya Choo hiyo kuna mabanda ya nyama choma, nyama ya Mbuzi inayochomwa vyema na wamasai. Ni tamu sana lakini hakuna maji ya kunawa wala vyombo vya kushikia nyama. Bongo tambalale.

Ni vyema mamlaka husika zikaangalia mazingira ya vituo vya kuchimba dawa ambavyo serikali iliagiza vijengwe baada ya kupiga marufuku abiria kuchimba dawa porini kwani ni uchafuzi wa mazingira. kwa hali ilivyo sasa mazingira ya vituo vya kuchimba dawa ni machafu zaidi kuliko maporini ambako abiria walikua wakichimba dawa kabla ya agizo la serikali.

Aidha Mamlaka husika zinapaswa kutupia macho pia katika hotel ambazo hupokea abiria wa mabasi kwa ajili ya chakula, iwe Chai, Chakula cha Mchana ama Chakula cha jioni kwa sababu sehemu nyingi hali ni mbaya, vyoo vilivyopo havikidhi idadi ya abiria wanaoingia, hakuna staha kwa sababu Mtoto wa Miaka sita nae huenda pamoja na watu wazima wa miaka 30 na kuendelea kujisaidia haja ndogo katika sehemu ya wazi ambayo mtoto anaweza kuona mipini ya watu wazima kitu ambacho sio kizuri na kinavunja heshima.

Pia usafi katika maeneo hayo una maswali mengi. Chonde chonde wataalamu angalieni jambo hili na chukueni hatua maana inaonekana kama vile ni kawaida and no one is taking action.

Naomba kuwasilisha.