Monday, June 3, 2013

Dk. Bilal afungua mkutano wa majadiliano kwa manufaa kwa wote, Dk. Nagu asema majadiliano ya Ushirikiano kwa wote ni kwa faida ya watanzania

IMG_8746 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (katikati) akisindikizwa na Katibu Mtendaji wa Baraza la Biashara la Taifa, Bw. Raymond Mbilinyi (kulia) wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kitaifa wa Majadiliano kwa manufaa ya wote jana jijini Dar es Salaam.
IMG_8783 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akihutubia wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kitaifa wa Majadiliano kwa manufaa ya wote ulioanza jana jijini Dar es Salaam.
EEE
Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
Serikali imesema Majadiliano ya Ushirikiano kwa Manufaa ya wote yanalenga kuwawezesha watanzania kumiliki uchumi wao na nchi kufikia uchumi wa kati kufikia mwaka 2025.
Akiongea na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam wakati wa siku ya pili ya mkutano wa Majadiliano ya Ushirikiano kwa Manufaa ya wote Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji na Uwezeshaji, Dkt. Mary Nagu alisema serikali imejipanga kuona majadiliano hayo yanaleta mapinduzi ya kiuchumi na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchumi wa viwanda katika eneo hili la Afrika.
“Serikali imedhamiria kuhakikisha majadiliano haya yanaleta manufaa kwa wananchi wake na majadiliano haya yanatoa msukumo wa kipekee kufanikisha hili,” alisema.
Dkt. Nagu ambaye alikuwa Mwenyekiti wa mkutano huo kwa niaba ya ya Makamu wa Rais, Dkt. Ghalib Bilal alisema serikali inataka kuona takwimu za kukua kwa uchumi wa nchi unaendana na maendeleo ya watu wake katika kila pembe ya nchi na kwa kila mtu.
Mkutano huu wa siku mbili uliomalizika jana ni matayarisho ya mkutano wa kimataifa wa Majadiliano ya Ushirikiano kwa Manufaa ya wote au “Smart Partnership Dialogue Global 2013” unaotarajiwa kufanyika mwezi Julai mwaka huu hapa Tanzania.
Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) kama taasisi ya serikali ilipewa jukumu la kuratibu majadiliano haya kitaifa. 
Akiwasilisha mada katika mkutano huo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Bw. Lucas Kusima alisema usalama wa nchi ni mtaji wa maendeleo hivyo kila mtu hana budi kulinda usalama wa nchi ili kufikia maendeleo ya kweli.
“Kama usalama haupo hakuna wawekezaji wala watalii watakaokuja,” alisema na kuongeza kuwa usalama ni muhimu katika kukuza ushirikiano wa kimataifa.
Alisema dalili za usalama kutoweka hapa nchini kama migogoro ya kidini, kisiasa, kugombea ardhi kati ya wafugaji na wakulima haina budi kutafutiwa suluhisho la kudumu kwa faida ya wananchi.
“Kuna umuhimu wa vyombo vya usalama kushirikiana na wananchi kuimarisha usalama wa taifa zima kama kweli tunataka majadiliano haya yalete manufaa,” alisema.
Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Saidi Mwema alisema wakati umefika wa makundi mbalimbali nchini kuunda kamati za ulinzi katika maeneo yao ili kujihakikishia usalama.
Akitoa mfano alisema maeneo ya ibada kama makanisa, misikiti, maeneo ya kazi, na majirani wanaweza kuunda kamati za ulinzi na jeshi la polisi liko tayari kuwawezesha mbinu mbalimbali za ulinzi katika maeneo yao.
“Jeshi la polisi linahitaji sana ushirikiano wa karibu na wananchi ili kufikia malengo ya usalama,” alisema.
Awali akifungua mkutano huo, Dkt. Bilal alipendekeza majadiliano hayo kuanza kufanyika kila mwaka hapa nchini ili kuharakisha maendeleo.
Dkt. Bilal alisema kwenye ngazi ya mikoa na wilaya majadiliano hayo yafanyike kila mwaka wakitumia mabaraza yao ya biashara ngazi husika kabla ya majadiliano ya kitaifa.
“Mabaraza ya biashara ya mikoa na wilaya yatasimamia utekelezaji wa mambo yaliyokubalika ngazi husika na kufanyiwa tathmini kila mwaka,” alisema.
Makamu wa Rais alisema kuwa majadiliano haya yanatoa fursa kwa viongozi wa serikali kukutana na kada mbalimba za wananchi ili kujadiliana na kuelewa mambo yanayochangia upatikanaji maendeleo endelevu.
Alieleza kuwa uzoefu unaonesha kuwa, mtu mmoja mmoja au makundi ya watu, wakishirikishwa na kuhamasishwa katika jambo lolote, na wakiliamini na kulikubali; utekelezaji wake huwa rahisi.
“Azma hii itatusaidia katika utekelezaji wa mipango yetu ya maendeleo ya miakamitano na dira ya maendeleo ya taifa ya 2025,” alisema.
Alitaja misingi ya majadiliano ambayo huleta maendeleo endelevu kama kuamini kwamba jirani wa mtu akiendelea basin a watu wote wanaendelea na kwamba maendeleo hayaji kwa kukwamishana na kulumbana bali kwa kushirikiana.
Alitaja msingi mwingine kuwa ni watu wote ni sawa bila kujali nyadhifa zao kwenye jumuia wanazoishi.
“Kila mtu anao mchango mkubwa katika kuleta maendeleo katika jumuiya anayoishi,” alisema.
Alisema kuna umuhimu wa kuachana na dhana potofu ambayo viongozi wa juu hutoa maagizo ngazi ya chini kwa utekelezaji na kuwa viongozi wakubali kupokea na kuthamini ushauri toka chini kwenda juu kwa utekelezaji.
Alitaja msingi mwingine kama ni kuwa na muono wa pamoja na utekelezaji wa nidhamu wa hali ya juu.
Kabla ya majadiliano haya TNBC iliendesha mikutano ya kuelimisha wananchi kupitia makundi mbalimbali kupitia katika jumla ya kanda 11; tisa Tanzania bara na mbili Tanzania visiwani mmoja Pemba na mwingine Unguja. 
Mkutano huo ulihudhuriwa na watu zaidi ya 500 wakiwemo viongozi wa serikali toka mikoa yote, vikundi mbalimbali na sekta binafsi.