Sunday, April 7, 2013

Aibu ya Mahakama Wilaya Bagamoyo

Umewahi kuingia ndani ya  Mahakama ya Wilaya ya Bagamoyo? Binafsi kwa mara ya kwanza niliingia Jumatano iliyopita, nikifuatilia kesi, kama ijulikanavyo kazi za waandishi wa habari. Nikiwa ndani ya ukumbi wa mahakama ya wazi, sikuamini nilichokishuhudia katika mji huo maarufu wa kihistoria, kitaifa na kimataifa; ikiwa ni pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete kuwa mzaliwa wa wilaya hiyo.
Hata Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Shukuru Kawambwa ni mbunge wa jimbo hilo lenye vivutio vingi vya kihistoria.
Macho yangu yakatua katika paa la mahakama hiyo na  kupokelewa na mabati yaliyotoboka-toboka, ilhali nyaya za umeme zikiwa zimetandazwa kupitia baadhi ya nguzo kwa minajili ya kusambaza umeme ndani ya jengo hilo.
Nikarejesha fikra zangu kwenye tukio la kuporomoka jengo lililokuwa na ghorofa 16  hivi karibuni jijini Dar es Salaam. Nikaanza kuingiwa hofu kutokana na baadhi ya kuta kusheheni viraka huku nyufa nyingine zikishindikana kudhibitiwa na viraka,  hali iliyosababisha kuta kuwa na michirizi  na hivyo kutoa taswira ya uchakavu wa jengo hilo.
Nikabadili uelekeo. Nikayaelekeza macho  upande wa kushoto kwangu, pembezoni  mwa vizimba, jirani na mlango unaotumiwa na hakimu kuingia mahakamani. Nikahisi kuishiwa nguvu baada ya kuona majalada yakiwa yamehifadhiwa katika eneo lisilo na mlango wala dirisha.
Panapotakiwa kuwa na dirisha, pamewekwa  mbao laini na kufunikwa kwa mapazia. Ikumbukwe hata kama majalada hayo ni ya kesi zilizoisha, haimaanishi kumbukumbu zake hazina maana.
Nikainamisha uso nikiwaza jinsi ya kutumia kalamu yangu angalau kutimiza wajibu wangu juu ya suala hili, macho yangu yakakutana na sakafu iliyochoka, ikiwa na nyufa za kutosha.
Kwa mujibu wa Katiba ya nchi, mahakama ni muhimili wa dola ambao  ngazi yake ya wilaya ina hadhi ya kupokea kesi za mauaji  yaliyo kwenye hatua za awali, wakili kutekeleza baadhi ya majukumu yao kushughulikia mashauri ya madai,  yenye thamani ya kuanzia Sh10 mil mpaka Sh100mil.
Katika hali ya kawaida, ilitarajiwa jengo linalotumika kwa shughuli za mahakama, liwe na hadhi inayoshabihiana na umuhimu, unyeti na usiri wake achilia mbali hadhi ya utu wa mtumishi wa umma.
Kwanini hali inakuwa hivi?
Gazeti hili lililazimika kuhojiana na uongozi kwa lengo la kujua kulikoni.Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Liad Chamshama anasema “Mahakama imekuwa moja ya waathirika wa mfumo wa mgawanyo wa rasirimali za nchi usiozingatia usawa, ukiwa makini utabaini serikali kuu inapendelewa zaidi ikifuatiwa na wanasiasa.”
Anabainisha kuwa ubovu wa jengo hilo nilioushuhudia si lolote, kwani hata Mhandisi wa wilaya hiyo ameishasema tena kwa maandishi kuwa halifai tena kwa matumizi.
Anasema ilifika wakati wakalazimika kufanya ukarabati mdogo kwa kubadilisha miti iliyoshika mabati kwenye paa wakaweka mbao, baada ya paa kuchakaa kiasi cha kufanya waache kuendelea na kesi mvua zinaponyesha.
“Hata sasa mvua ikinyesha inabidi niwaruhusu watumishi wakapumzike tu nyumbani maana maji yanajaa eneo lote la mahakama, hapo nje kuna matofali yamepangwa, mvua isipokuwa kubwa huwa tunayatumia kama njia ya kuingilia mahakamani,”anafafanua Chamshama
Hata hivyo anasema kwa kushirikiana na Mkuu wa wilaya hiyo, Ahmed Kiponzi wanaendelea kujadiliana namna ya kujikwamua kutoka kwenye hali hiyo.
Anatoa wito kwa mamlaka zinazohusika kuhakikisha kunakuwa na mgawanyo sawa wa rasilimali, ili kuweka ufanisi mzuri katika uwajibikaji wa mahakama kwa ujumla.
Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu, Kiponzi anakiri kuwa suala hilo ni nyeti na lenye kuwafikirisha, kwamba atakapokutana ana kwa ana na gazeti hili ataeleza mipango iliyopo.
Mbunge wa jimbo hilo na waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Shukuru Kawambwa anasema miongoni mwa mambo yanayomuumiza kichwa ni maboresho ya jengo hilo la mahakama ya wilaya na kwamba jitihada zake zimekuwa zikikwama kutokana na ufinyu wa bajeti ya wizara ya Sheria, Katiba na Utawala.
Kilo Khamis Mdete (42) mkazi wa Bagamoyo anayejishughulisha na kilimo kijijini Miono, akizungumzia hali ya mazingira ya mahakama hiyo ambapo alifika kusikiliza kesi yake ya mgogoro na wafugaji, anasema:
“Siyo siri hii ni aibu, mimi sikusoma ningekuwa nimesoma nina shahada yangu nisingekubali kuletwa nifanye kazi kwenye ofisi kama hii. Hata mtu kutoa rushwa ni rahisi kwa kuwa mazingira yanaashiria waliyomo wana njaa kali.
Ofisi ikiwa nzuri, mtu anakuwa na heshima na watumishi wanaofanyia kazi humo wanaheshimika, hata wazo la kutoa rushwa likimjia mtu anahofu kwasababu atajiuliza mara mbili atoe shilingi ngapi, hatimaye atahamasika kubaki kwenye mstari wa sheria,” anasema Mdete.
Baadhi ya wananchi wanalalamikia dharau za viongozi wakisema kuwa hawaoni umuhimu wa kuboresha mahakama nchini, kwani zaidi ya majengo hata malipo mazuri imekuwa ni tatizo.
Habari na Editha Majura  
Chanzo - Mwananchi