Sunday, April 7, 2013

Mkapa atema cheche; ataka viongozi wafuate misingi ya Nyerere

  

Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa amesifia utawala wake kwa kuongoza taifa bila ya kubaguana na amesikitishwa na matukio ya udini, ambayo yanaashiria kuvuruga amani na utulivu wa Tanzania katika siku za karibuni.
Akitoa salamu zake baada ya kusimikwa kwa Askofu Mpya wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Desdelius Rwoma, Mkapa alisema anachojivunia ni kuheshimiwa na waumini wa madhehebu yote.

“Katika kipindi cha uongozi wangu, viongozi wa madhehebu yote walikuwa wakinisisitizia kuwa sisi sote ni ndugu pamoja na tofauti zetu za kiimani. Wakati wa utawala wangu nilijitahidi kwa uwezo wangu wote kuwahudumia wananchi bila kuwepo kwa malalamiko ya kubaguana katika jamii,” alisema Mkapa, ambaye aliiongoza Tanzania kuanzia mwaka 1995-2005.

Mkapa alionya kuwa taifa limeacha misingi aliyoiacha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ambaye mara zote alisimamia umoja wa taifa.

“Wakati wa utawala wangu nilijitahidi kwa uwezo wangu wote kuwahudumia wananchi bila kuwepo kwa malalamiko ya kubaguana katika jamii,” alisema.

Mkapa ambaye hakupanga kuongea lolote katika tukio hilo, alitaka taifa lijenge utamaduni wa kupendana, huku akilaumu kuwa kizazi kipya cha uongozi kimeanzisha mambo ya ajabu ya kukosa upendo na kudhalilishana.


Pia alitahadharisha kuwa zama hizi kumeibuka mitafaruku mbalimbali na kuwakumbusha Watanzania kuwa ni wakati wa kumwabudu Mwenyezi Mungu.

Mkapa alisema mara nyingi alishauriana na viongozi wa dini katika masuala ya kijamii na kiroho na kumtaja askofu mpya wa Bukoba, Rwoma na Mtangulizi wake aliyestaafu Nestory Timanywa kuwa alishirikiana nao katika masuala ya wananchi. Onyo la Mkapa limekuja siku chache baada ya Rais Jakaya Kikwete kukemea mambo ya kidini na kutetea Serikali yake haiongozi kwa misingi ya ubaguzi.

Katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi, Rais Kikwete alikwenda mbali zaidi na kudai amekuwa akilalamikiwa na viongozi wa madhehebu ya Kikristo na yale ya Kiislamu.

Maneno ya Mkapa na Kikwete yamekuwa katika kipindi hiki taifa likiwa limetikiswa na matukio yenye mwelekeo wa chuki za kidini. Matukio makubwa yakiwa yale ya kuuawa wa Padri Evarist Mushi huko Zanzibar na Mchungaji Mathayo Kachila wa Geita.

Pia kupigwa risasi kwa Padre Ambrose Mkenda na kumwagiwa tindikali kwa Sheikh Fadhil Soraga na vurugu za mambo ya kuchinja huko Geita na Tunduma.

Askofu Mpya wa Bukoba Rwoma alimshukuru Mkapa kwa kuzungumzia umuhimu wa amani ya nchi, huku akisisitiza suala la upendo miongoni mwa wananchi.